Rambirambi zatolewa kufuatia kifo cha Bi. Kibaki
Yafuatayo ni baadhi ya matukio yaliyogonga vichwa vya habari nchini Kenya siku ya Jumatano Aprili 27, 2016 kama tulivyo yapokea katika chumba chetu cha habari.
Gavana Lusaka atoa risala za rambirambi kufuatia kifo cha Bi Lucy Kibaki
Gavana wa kaunti ya Bungoma Kenneth Makelo Lusaka ametuma risala za rambirambi kwa Rais mstaafu Mwai Kibaki kufuatia kifo cha mkewe Bi Lucy Kibaki kilichotokea siku ya Jumanne katika hospitali ya Bupa Cromwell jijini London, Uingereza.
Ujumbe wa makiwa sawia na huo ulitolewa na Mbunge wa Kaunti ya Trans Nzoia, Janet Nangabo aliyemsifia marehemu akitoa wito wa wanawake kote nchini kuiga mfano.
Mkewe Rais Mstaafu Mwai Kibaki, Lucy Kibaki alifariki Jumanne akipokea matibabu jijini London.
Katika kumbukumbu ya kumuomboleza Bi Kibaki, Rais Uhuru Kenyatta alimsifu kwa jukumu lake la kukabiliana na ugonjwa wa ukimwi nchini kenya.
Rais Kenyatta alisema marehemu aliugua kwa kipindi cha mwezi mmoja uliopita ambapo amekuwa akipata matibabu nchini Kenya na Uingereza.
Viongozi mbalimbali ikiwemo wabunge wamemtaja Bi Lucy kama kiongozi mkakamavu na aliyewajali wanawake na kuwatia motisha kila mara.
Viongozi wa mrengo wa CORD hawakuachwa nyuma wakimtaja Bi Kibaki kama aliyesaidia sana katika serikali ya muungano.
Mwendazake alizaliwa mnamo mwaka 1940.
Awali alifanya kazi ya ualimu.
Chuo cha kiufundi cha Naitiri chapokea ufadhili wa ujenzi wa bweni
Shughuli za elimu katika chuo cha kiufundi cha Naitiri katika wadi ya Mbakalo zimepigwa jeki baada ya serikali ya kaunti ya Bungoma kukipa ufadhili wa shilingi millioni moja kufadhili ujenzi wa bweni.
Serikali ya Bungoma yatakiwa kuweka taa Khachonge kupunguza uhalifu
Mwakilishi wa wadi ya Luhya Bwake eneo bunge la Kabuchai Rosemary Khisa ameitaka serikali ya kaunti ya Bungoma kuweka taa katika soko la Khachonge ili kusaidia kupunguza uhalifu unaotishia wafanyibiashara wengi eneo hilo.
Wazazi wa zeruzeru watakiwa kuwalinda dhidi ya unyanyapaa
Wazazi walio na watoto wanaoishi na ulemavu wa ngozi, wametakiwa kuwalinda msimu huu wa likizo kama njia moja ya kuzuia visa vya unyanyapaa dhidi yao.
Ukeketaji wa wasichana Pokot bado donda dugu
Licha ya serikali kuweka adhabu kali kwa wale wanaowakeketa wasichana nchini, jamii ya Pokot bado haijapiga hatua kubwa katika vita dhidi ya ukeketaji. Haya ni kwa mujibu bodi ya kupambana na ukeketaji nchini.
Shule ya upili ya Lutacho yahitaji bweni jipya
Wito umetolewa kwa viongozi, washika dau na wahisani kujitokeza na kuisaidia shule ya upili ya Lutacho kujenga bweni jipya baada ya moto kuteketeza bweni shuleni humo miezi mitatu iliyopita.
Askari wa magereza azuiliwa Bungoma kwa shutuma za hongo
Polisi mjini Bungoma wanamzuilia mtu mmoja anayedaiwa kuwa askari wa magereza kwa kupatikana akichukua hongo kutoka kwa baadhi ya wakaazi katika hoteli moja mjini Bungoma mbele ya usajili wa makurutu wanaotarajiwa kujiunga na kikosi cha maafisa wa magereza Jumatano hii.
Mtuhumiwa huyo alikamatwa usiku wa kuamkia Jumatano hii baada ya polisi kupashwa habari na wananchi.
Maafisa wa upelelezi waliwafumania maafisa hao wengi wao wakidaiwa kutoka Kakamega na Bungoma japo wengi wao walifanikiwa kutoroka.
Walimu Kakamega wahimizwa kuingia katika siasa
Walimu katika kaunti ya Kakamega wametakiwa kujitokeza na kuwania viti mbalimbali vya kisiasa katika uchaghuzi mkuu ujao, ili wapate viongozi watakaoyashughulikia na kutetea matakwa yao.
Trump ashinda mchujo wa kutea mgombea uraisi Marekani
Donald Trump ameshinda mchujo wa kuteua mgombea urais wa chama cha Republican katika majimbo matano ya marekani yaliyopiga kura Jumanne.
Kwenye Spoti
Wadhamini wakuu wa timu za AFC Leopards na Gor mahia Sporstpesa wametupilia mbali udhamini huo kwa kigezo cha rabsha zinayosababishwa na wafuasi wa vilabu hivyo.
Klabu ya Manchester city yalazimisha sare ya kutofungana goli didi ya Real Madrid kwenye nusu fainali ya kwanza ya ligi ya mabingwa ulaya.